Get in Touch

Definition List

Pages

Translate

Friday, January 25, 2019

Tuhuma za Zitto na Funzo la Bruce Lee, Lissu na Julius Caesar

ZITTO KABWE

Tuhuma za Zitto na Funzo la Bruce Lee, Lissu na Julius Caesar
Na Munir Abubakar, Dar es Salaam
HIVI karibuni nimemsikia Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe, akiibuka na tuhuma za ajabu kwa mwanasiasa wa aina yake kuzitoa; kwamba ametishiwa maisha akiwa Bungeni tena akituhumu watu wa Idara muhimu katika kulinda usalama wa nchi hii.

Kauli ya Zitto si ya kwanza kwa wanaofuatilia mambo mengi anayoyaandika kwenye mitandao mbalimbali ya kijamii. Mara kadhaa amekuwa akiibuka na kuzusha madai kama hayo akidai kuna watu wanapanga njama za kumuua na mara zote akiitaja Serikali.

Kama madai yake hayo yanaukweli au ni “kiki” za kisiasa ni suala linalohitaji utafiti wa kina ambao aghlabu makala haya kwa sasa hayawezi kufikia hitimisho, lakini kama Taifa yako mambo lazima tuungane kuyakataa; hasa tabia hii mpya ya kila mwanasiasa kuibuka tu na madai ya jumla jumla kuwa Serikali au vyombo vyake vinatak kumdhuru.

Niseme tu, kauli ya Zitto, ambaye inadaiwa amelifikisha suala hilo la jinai kwa Spika wa Bunge, badala ya Polisi, ni mwendelezo wa staili mpya hapa nchini ya wanasiasa wanaoonekana kuishiwa hoja za kisiasa kukimbilia kudai wanatishiwa na Serikali au vyombo vyake.

Haraka haraka niliposikia kauli ya sasa ya Zitto na anavyoendelea kulishadidia suala hilo mitandaoni, nikakumbuka hadithi nyingi juu ya yaliyowafika wanasiasa wengi duniani huko nyuma katika maisha yao ya kisiasa ambapo madhara mengi waliyoyapata ilikuja kubainika kuwa hayahusiani ni kile wengi walichoamini au kuaminishwa awali.

Nasisitiza sikatai kuwa Zitto anaweza kutishiwa na taasisi au mtu binafsi katika Serikali, hilo ni suala la mahusiano na ushahidi, lakini nasisitiza pia tusikatae kuwa Zitto huyo huyo anaweza kuwa na “bifu” mbaya zaidi zinazohatarisha maisha yake na makundi mengine ya watu wasio Serikali, lakini kisiasa, kila siku akawa anaonesha adui yake ni Serikali tu.

Katika kuyaelewa anayoyaleta Zitto hapa nchini hivi sasa, nimelazimika kuirejea upya fasihi niliyopata kuisoma zamani ya mwanahistoa za masuala ya madhara ambayo viongozi mbalimbali wa kisiasa wamekuwa wakiyapata J. Bowyer Bell, aliyeandika tasnifu Assassin: Theory and Practice of Political Violence. 1st Edition.”

Tasnifu hii inatusaidia kuyaelewa madhara mbalimbali ambayo yamepata kuwakumba wanasiasa duniani na sababu tofauti ambazo wakati fulani, baada ya uchunguzi, ilibainika kuwa ni tofauti kabisa na sababu ambazo watu waliamini au waliaminishwa kama Zitto anavyofanya hapa nchini.

Ni ukweli uliodhahiri kuwa Zitto ana maadui wengi na wanajulikana. Ni vyema akaishi kwa kujitathmini maisha yake badala ya kila mara kulaumu Serikali. Mfano, bado usaliti wake kwa Chadema umeacha alama isiyofutika, kuna makampuni/nchi mbalimbali ambazo amekuwa anawatumikia kisiasa na kuna wakati anabadilika na kuibua bifu lakini kijamii, anajulikana, niseme tu kuwaumiza mabinti wengi.
Nimetaja baadhi ya “facts” tu zinazoweza kutusaidia kuyaelewa matishio aliyonayo Zitto hasa wakati huu pia yeye na baadhi ya wanasiasa wa upinzani wanapogongana kuweka nia za kuwania Urais, kwa sababu bahati mbaya yeye bado anatangaza tu kuwa adui wake ni Serikali.

Labda tumkumbushe Bw. Zitto anachokifanya leo hapa Tanzania kimeshatoke katika kioo halisi cha maisha ya wanasiasa na watu wengine wengi mashuhuri ambapo kile ninachokisema kuwa mtu anaweza kuwa na maadui wengi na yeyote kati yao akamdhuru kilisadifu. Nitatoa mifano michache.

Kama Zitto anavyotaka kutuaminisha, akiwa amewaudhi Waislamu wa India na kila mtu akiwa anajua adui mkubwa wa Gandhi yangekuwa makundi yenye msimamo mkali wa kiislamu, siku ya Januari 30, 1948 alipouawa Mahatma Gandhi wa India na kijana wa dhehebu lake la Kihindu aitwae, Nathuram Vinayak Godse, ndipo watu walipopigwa na butwaa!

Hadithi ni kama hiyo ya Zitto kwa mtaalamu wa filamu za Kung Fu na mwasisi wa mtindo wa mapigano wa Jeet Kune Du, Bruce Lee ambaye kila mmoja alijua maadui zake ni wahafidhina wa Kichina waliokuwa hawataki afundishe sanaa hiyo ya Kichina kwa Wamarekani.

Lakini kumbe, tofauti na adui huyo ambaye hata Bruce Lee alikuwa akimtangaza hadharani, adui halisi aliyekuja kuhitimisha maisha yake akabainika ni afya yake, tabia yake ya kutopumzika na mazoezi ya nguvu. Ndio maana mabingwa wote wa tiba wakathibitisdha kuwa Julai 20, 1973 alipofariki usingizini, kilikuwa kifo kilichotokana na madhara hayo katika ubongo na dawa alizokunwa.
Lakini yapo pia mafunzo kuhusu mauaji ya aliyekuwa Waziri Mkuu wa Israeli Yitzhaki Rabin ambaye maadui wanaoisaka roho yake wangeweza kuwa Wapalestina waliokuwa wanaona wanaonewa lakini na wanasiasa wenzake wa chama cha upinzani cha Likud.

Lakini siku anauawa Novemba 4, 1995 na kijana wa Kiyahudi, Yigal Amir, ndipo dunia ikajua tu kwamba kumbe mitazamo tofauti ya kisiasa na siasa za ushindani zinaweza kumtengenezea mwanasiasa maadui miongoni mwa vijana na watu wa kawaida.

Tunajifunza pia kutoka kifo cha mtawala wa zamani wa Roma Julius Caesar, ambaye baada ya kujikinga kwa muda mrefu na husda za maadui zake wa nje ya Dola ya Rumi aliyokuwa ameijenga kwa mabavu, ni washirika wake wa ndani kisiasa (maseneta akiwemo kijana wake Brutus) waliosshiriki kumuua kwa kumchoma visu 23 akiwa kwenye jumba la Maonesho la Pompey (Pompey Theatre mnamo mwaka 44BC).

Hoja yangu hapa ni kwamba Zitto aache kuudanganya umma kwanza kwa kila mara kuonesha kuwa ana adui mmoja tu; Serikali ili siku maadui wengine wakimdhuru au akinusurika na madhara hayo Serikali ichafuke. Hii ni kiki ya kijinga sana ya kisiasa.

Wakati mpaka leo wengi bado wanatafakari ni nani hasa amehusika kumdhuru Tundu Lissu, ninachokiona, na ambacho naamini hata wachunguzi wa suala la Lissu inawachukua muda ni tabia hii hii ya wanasiasa wetu nchini kuficha madhambi au maadui zao wengine na kuuandaa umma kujua adui wao ni mmoja tu; Serikali.

Kama Zitto anavyotamani umma umwanini, tumeona katika sakata la Tundu Lissu naye wakati huo na hata sasa amejaribu sana kuuhadaa umma ionekane kama vile Serikali ndiyo adui wake pekee ili linapomtokea lolote, Serikali ichafuke.

Kama ambavyo leo tunamuona Zitto anaanza kwa mara kadhaa kurudia rudia kuwa eti kuna maafisa wa Serikali wanapanga mkudhuru, Lissu naye alianza kwa lawama hizo hizo, mara akitoa namba za gari aliyodai inamfuatilia na kudai ni la Serikali mara kaamka tu kitandani Nairobi hata akiwa hajui tarehe ya siku hiyo akaanza kuropoka ni Serikali.

Nafahamu, kwa kuwa wote nimebahatika kuwa karibu na familia zote, wote, Zitto na Lissu, wanamatishio mengi kwa maadui zake kadhaa na najua wataalamu wa Serikali wenye uwezo wa kuona zaidi ya tunayoyaona, wameshapata kuwaonya wachukue hatua au wapewe msaada ulinzi, wamekuwa wakikataa.

Ni kwa sadfa au bahati mbaya tena, wanasiasa hawa wawili, pamoja na kukataa ushauri au ofa ya kupatiwa msaada wa ulinzi, kwa mujibu wa duru za familia zao, na huku wakijua hatari walizonazo kutokana na njama za maadui zao, wamekuwa na kiburi cha kisiasa cha kuendelea kuitusi na kuituhumu Serikali.

Mtu angeweza kujiuliza kwa nini Zitto bado anaona kuna faida kuilaumu Serikali wakati anajua matisho ya sababu nyingine aliyonayo? Jibu la utafiti wangu ni kwamba wanaomjua kisiasa Zitto Kabwe watakubaliana nami kuwa ni kweli sio yule wa zama za Buzwagi.

Amechuja sana na kama kuna jambo amebaki nalo kwa sasa baada ya zile zama za kuibua ufisadi mkubwa mkubwa na kwa ushahidi mzito kwisha, basi ni kuokoteza okoteza hoja walau aonekane bado yupo katika siasa. Hivyo anahaha kusaka kiki za kisiasa.

Yule Zitto Kabwe wa Daruso na Zitto Kabwe wa Buzwagi, mwanasiasa kijana aliyekuwa upande wa wanyonge na upande wa maendeleo sio wa sasa. Mazingira na hali halisi vimemfanya kwa sasa alazimike kuwa upande wa mabeberu akiwaunga mkono katika mambo mbalimbali. Hivyo maisha yake nchini yamebaki ya kuungaunga kisiasa. Kuitaja Serikali kuwa inataka kukudhuru yeye anaona kunalipa!

Nimesema hapo awali kuwa kuna kauli anazitoa kwa sasa Zitto zinafikirisha na ni vyema sisi Watanzania tukazitafakari kwa kina. Zitto anatamani kutembelea katika nadharia ya Lissu; kwamba kwanza aanze kuonesha huruma kuwa kuna watu wanataka kumdhuru, ili siku likimtokea kweli, iwe kwa sababu yoyote, ilaumiwe Serikali na kila mtu awe upande wake.

Kama alivyoanza Lissu, sasa hivi unamuona Zitto naye mara kwa mara anatamka kuwa “amesikia” mara “ameelezwa” kuwa kuna mipango ya maafisa wa Serikali kumdhuru. Hadithi hizi zinapita mule mule kwenye mikono ya Lissu, kwenye dhana ya Bruce Lee na kwenye akili na maisha ya wafuasi wa Gandhi na wale wa Rabin.

Hapa nisipoteze, ninachokiona hakuna cha Usalama wa Taifa wala nini, Zitto anakoleza stori kuhalalisha kiki yake ya kisiasa ili ikitokea akajidhuru, kudhuriwa na maadui zake wengine au lolote likamtokea moja kwa moja ailaumu Serikali kama njia ya kupanda chati tena.

Nionavyo, kwa sasa hatupaswi kuendelea kulea usanii wa aina hii, niwaombe tu Watanzania tukatae majaribio yoyote yenye lengo la kisiasa kuipaka matope nchi yetu, tukatae wanasiasa hawa ambao wako tayari kudhurika au kutunga kudhurika au kuficha madhambi waliyonayo ambayo yanaweza kuwa chanzo cha kudhurika kwao ilimradi tu ikitokea waichafue nchi yetu. Tukatae. Tusikubali. 

No comments: